SUMAYE:HAKUNA MWENYE MAMLAKA YA KUTOA ROHO YA MWENZAKE,ALIA NA MATUMIZI MABAYA YA SILAHA

sumaye1 12547
Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye ameelezea kushangazwa na mauaji yanayotokea mara kwa mara nchini, akisema kuwa hakuna mwenye mamlaka ya kutoa roho ya mtu. (HM)
Sumaye alitoa kauli hiyo jana katika Usharika wa Kimashuku wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) wakati wa harambee ya kuchangia fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa kanisa hilo.
"Mtu anarudi nyumbani na anapofika getini anauawa wakati hakuna mahali katika vitabu vitakatifu kuna maelekezo ya baadhi ya watu kuwa na haki ya kutoa roho za wenzao," alisema Sumaye.
Katika harambee hiyo ambayo ilihudhuriwa pia na Askofu Mstaafu wa Dayosisi ya Kaskazini ya KKKT, Dk Erasto Kweka na viongozi mbalimbali wa dini na kisiasa, Sumaye alichangia Sh1 milioni.
Akizungumzia suala la rushwa, alisema hivi sasa Tanzania inaongoza kwa rushwa eneo la Afrika Mashariki na kama hatua za haraka hazitachukuliwa kuidhibiti nchi itaikaribia Nigeria.
Kanisa hilo lililopo Mailisita wilayani Hai mkoani Kilimanjaro, linahitaji Sh400 milioni kwa ajili ya kukamilisha kazi ya ujenzi.
Sumaye alisema kuongezeka kwa matukio ya mauaji kwa watu wasio na hatia ni matokeo ya kumomonyoka kwa maadili. Sumaye alisema ni jambo linalotaka kuzoeleka nchini kwamba, mwananchi anapohitaji huduma ni lazima adaiwe rushwa ili kupata huduma huku wengine wakinyanyaswa kijinsia. Chanzo: Mwananchi
 
© 2012. Design by Ernest James Siwigo Chambasi - Supported By John James Chambasi And Maganza Family