WANANCHI WAIPONGEZA SERIKALI KWA KANUNI ZA KUSIMAMIA BIASHARA YA GESI

BAADHI ya wananchi wameipongeza Serikali kupitia Wakala wa Vipimo (WMA) kwa kuanzisha kanuni ya kusimamia biashara ya gesi ya kupikia iliyofungashwa kwenye mitungi na inatotumika sana nyumbani na hotelini (LPG) na kusema kuwa hatua hiyo inalenga kuboresha maisha yao na hatimaye kupunguza uharibifu wa mazingira.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi hao wanasema kabla ya kanuni hiyo kutungwa ilikuwa ni vigumu sana kwao kufahamu haki zao wanapokwenda kununua gesi hiyo ya mitungi, kwani kanuni haikuwa wazi kuhusu biashara hiyo.
Rehema Tendwa wa Dar es Salaam anasema iwapo kanuni hiyo itatekelezwa ipasavyo itachochea ukuaji wa biashara hiyo kutokana na wananchi kuwa na imani na huduma wanayoipata kutokana na ujazo wa gesi kwenye mitungi kulingana na thamani ya pesa yao na hivyo matumizi ya nishati ya mkaa na kuni kupungua na hivyo kusaidia kutunza mazingira yetu.
Shabu Kibaja wa Temeke ambaye amekuwa akitumia gesi kwa muda mrefu kupikia, anaona kuwa kanuni hiyo itatekelezwa kikamilifu, ni dhahiri wateja wa mitungi hiyo wataweza kupata haki yao.
Rashid Bwela wa Kibaha mkoani Pwani anasema: “Kuna makampuni mengine yanayouza gesi yanaweka gesi kidogo kwenye mitungi yao wakati kuna mengine angalau yanaweka ya kutosha, yaani biashara hii ni holela, na hakika kwamba kanuni hiyo itatusaidia kuwa na huduma moja inayoeleweka.”
Beatus Kapama, mkazi wa Ukonga Jijini Dar es Salaam, anaipongeza serikali kuwa kuchukua hatua hiyo katika kipindi hiki. Anasema biashara hiyo imeshamiri kutokana na maendeleo ya kiuchumi yanayotokea hapa nchini kwa sasa na pia itasaidia katika kupunguza uharibifu wa mazingira.
“Kwa kweli kanuni hii imekuja wakati muafaka, wananchi wengi wanatumia gesi tofauti na hapo awali ambako walikuwa wanatumia mkaa na kuni, hivyo kuchangia uharibifu wa mazingira kwa kweli kuna maendeleo, hivyo uwepo wa kanuni inayosimamia biashara hiyo ni jambo jema sana kwani pia biashara hiyo itakua zaidi,”anasema.
Mwajuma Ally, Mkazi wa Unguja, Zanzibar, anaipongeza serikali kwa kuanzisha kanuni hiyo na kwamba inalenga katika kumkomboa mnyonge, hususan mwanamke ambaye ndiye husumbuka sana na kuni. “Ni kanuni muafaka kwa kweli inatulenga sisi watu wa hali ya kawaida, hususan mwanamke na iwapo itatumika vizuri ni dhahiri kwamba haki zetu kama watumiaji wa gesi majumbani zitalindwa,” anasema.
Mwajuma ambaye anasema kupikia gesi kuna raha kulinganisha kuni na mkaa, anaomba uwepo utekelezaji wa makini wa kanuni hiyo ili kuhakikisha kwamba malengo ya utungwaji wa kanuni hiyo yanatekelezwa. John Masanja mkazi wa Mwanza naye anasema kwamba serikali imeleta kanuni muafaka na kwa muda muafaka.
Akiongea kwa simu, Masanja anasema: “Hizi biashara za gesi zinazidi kukua kila kukicha naona serikali imekuja na kanuni muafaka kabisa. Naipongeza na ninaomba wote tushirikiane katika kuitekeleza”. Simon Mwakasege, Mwanasheria wa Jijini Dar es Salaam anaipongeza serikali kwa kuanzisha kanuni hiyo na kusema kwamba itasaidia kudhibiti biashara holela ya gesi hapa nchini.
“Nadhani kanuni hii italeta usawa katika biashara hii ya gesi hapa nchini. Wakati kulipokuwa hakuna kanuni wananchi walikuwa hawajui usahihi kabisa wa vipimo katika biashara hii, walikuwa na imani tu kwamba kampuni hii wanajaza gesi vizuri, wale wanapunja, basi, ilimradi tu ilikuwa ni vurugu, hivyo ni matumaini yangu kwamba kanuni hii itasaidia kuleta usawa katika biashara hii,” anasema.
Anasema kutokana na kukua kwa matumizi ya bidhaa za gesi hapa nchini ni dhahiri kwamba kanuni maalumu ni lazima iwepo ili kuwalinda watumiaji na hata wauzaji. Waziri Mkuu Mizengo Pinda amesema Tanzania inapoteza kiasi cha hekta 400,000 za misitu kila mwaka kwa sababu ya ukataji miti unaochochewa na matumizi ya kuni, mkaa, mbao, ujenzi ama uchomaji moto misitu.
Akizungumza hivi karibuni Mkoani Rukwa katika maadhimisho ya Siku ya Mazingira duniani, Pinda alisema utafiti uliofanywa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Mradi wake wa Tathmini ya Rasilimali za Misitu unaonesha kuwa ukataji huo wa misitu unasababisha kuzalishwa kwa tani milioni moja za mkaa ambao nusu yake unatumiwa na wakazi wa Jiji la Dar es Salaam.
“Tanzania inakadiriwa kuzalisha kiasi cha tani milioni moja za mkaa kila mwaka, nusu yake, yaani tani 500,000 zinatumika Dar es Salaam peke yake. Kuni zinatumika sana vijijini wakati mkaa unatumika sana mijini. Ndiyo sababu tunasisitiza kwamba, kama tukiwapatia wakazi wa mijini hususan wale wa Dar es Salaam nishati mbadala kama vile gesi, umeme na nishati itokanayo na jua, tutakuwa tumepunguza kwa kiasi kikubwa ukataji miti nchini kwa ajili ya kutengeneza mkaa,” anasema.
Baadhi ya wabunge wameitaka serikali kuhimiza matumizi ya nishati mbadala, ili kupunguza athari za mazingira zitokanazo na matumizi ya kuni na mkaa kwenye maeneo ya mijini na vijijini. Wabunge hao Diana Chilolo, Magdalena Sakaya (viti Maalum) Juma Kilimba (Iramba Magharibi), wanasisitiza umuhimu wa nishati mbadala kama vile gesi ya kupikia majumbani.
Wabunge hao wanasema kwa kiasi kikubwa mazingira yamekuwa yakiharibiwa kutokana na ukataji miti kwa wingi kwa matumizi ya nishati na hivyo kusababisha ukame. Wanaishauri serikali kuhimiza matumizi mbadala ya nishati kwa matumizi ya majumbani ili kukabiliana na uharibifu mkubwa wa mazingira.
Hivi karibuni serikali kupitia WMA, imepitisha kanuni ya kusimamia biashara ya gesi ya majumbani na hotelini ili kukabiliana na upungufu yaliyojitokeza katika uendeshaji wa biashara hiyo hapa nchini. Wakala wa Vipimo (WMA) ulioko chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara, jukumu lake kubwa ikiwa ni kumlinda mlaji kupitia usimamizi wa matumizi sahihi ya vipimo katika biashara, afya, usalama na mazingira.
Kazi kubwa ya WMA ni kuhakikisha kwamba vipimo vya bidhaa zinazouzwa kwa mteja zinalingana na thamani ya pesa yake. Mbali na kupitisha kanuni hiyo, serikali imekuwa ikisisitiza umuhimu wa nishati mbadala kama vile gesi ya kupikia majumbani ili kukabiliana na uharibifu wa mazingira unaosababishwa na matumizi makubwa nishati ya mkaa na kuni.
Magdalena Chuwa ni Ofisa Mtendaji Mkuu wa Wakala hiyo yenye Makao yake Makuu katika jengo la Mwalimu lililopo mtaa wa Uhuru, Ilala, jijini Dar Salaam.
Anasema pamoja na jukumu la uhakiki wa vipimo vya bidhaa mbalimbali ambao unafanywa na wakala wake, kwa miezi kadhaa iliyopita wakala ulielekeza nguvu zake katika kuandaa kanuni watakayotumia kusimamia vipimo vya matumizi ya gesi ya kupikia na anasema ni jambo la faraja kuona kwamba kanuni hiyo sasa inaanza kutumika rasmi.
Awali ya yote anatoa shukrani kwa wadau mbalimbali walioshiriki katika zoezi hilo muhimu na kwamba mawazo yao yalisaidia sana katika kufanikisha upatikanaji wa kanuni hiyo. “Lengo la kuiandaa kanuni hiyo ni kuhakikisha kwamba watumiaji wa gesi ya kupikia, wasambazaji na wadau wengine wote wanatumia vipimo sahihi kwa mujibu wa sheria za nchi ili Tanzania iweze kunufaika na rasilimali hii muhimu katika uchumi wake,” anasema.
Chuwa anasema hatimaye Kanuni hiyo imekamilika na tayari imeanza kutumika. Anasema kwamba kanuni hii imekamilika baada ya kuwashirikisha wadau mbalimbali ambao kwa kupitia vikao kadhaa walitoa maoni yao na baadaye kufanyiwa kazi ipasavyo na Wakala wa Vipimo kwa kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara.
Wakala wa Vipimo (WMA) ambao kazi yao ni pamoja na kusimamia matumizi sahihi ya vipimo katika biashara, walikuwa wakiandaa kanuni itakayosaidia kusimamia uuzaji wa gesi hiyo inayotumika majumbani kwa ajili ya kupikia.
Chuwa anafafanua kuwa Kanuni hiyo imesainiwa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda na tayari inatumika baada ya kutangazwa katika gazeti la serikali (GN) No. 222 la tarehe 19/07/2013 Anasema LPG ni aina ya gesi inayotokana na bidhaa za petroli ambayo huagizwa kutoka nje ya nchi kupitia makampuni yanayoagiza mafuta au bidhaa za petroli.
“Husafirishwa kwa meli na kupakuliwa kupitia mabomba maalumu na hatimaye kuhifadhiwa katika matangi makubwa kabla ya kupakiwa/kujazwa kwenye mitungi midogo midogo yenye uzito tofauti tofauti tayari kusambazwa kwa watumiaji. Chuwa anazidi kusema: “Ni ukweli usiopingika kuwa, hivi sasa nishati ya gesi imechukuwa nafasi kubwa sana katika jamii kwa matumizi ya kupikia majumbani kutokana na nishati nyingine kama kuni, mafuta ya taa na hata umeme kuwa na gharama za juu sana au upatikanaji wake kutokuwa wa uhakika.
Kutokana na hali hiyo, gesi imekuwa biashara kubwa nchini na hivyo kusababisha makampuni mengi hasa yale yanayosambaza nishati ya mafuta kujiingiza pia katika biashara ya gesi ya kupikia ili kukidhi mahitaji ya soko.
“Ni matarajio ya Serikali kuwa biashara ya gesi hususani ya majumbani itafanyika kwa kuzingatia Sheria ya Vipimo pamoja na Kanuni zake, hasa katika eneo la vipimo vya uzito wa mitungi ya gesi ili kuhakikisha kwamba msambazaji na mtumiaji kila mmoja anapata haki yake kulingana na thamani ya pesa yake.”
Chuwa anafafanua kuwa uchunguzi uliowahi kufanywa na Wakala wa Vipimo ulikuwa umebaini kuwa baadhi ya wafanyabiashara hasa mawakala walikuwa wanatumia ujanja katika kujiongezea faida kwa kupunguza uzito wa mitungi ya gesi na kupakia katika mitungi midogo midogo.
Aidha, uchunguzi huo ulibaini pia mapungufu mengi ya kiufundi, mfano ulikuwa ukiangalia mitungi ya gesi ya kupikia (LPG) ilivyoandikwa utaona kuwa kila kampuni inayosambaza gesi kwa matumizi ya majumbani imekuwa ikiandika taarifa katika mitungi yao kwa jinsi wanavyojua wao na hivyo kuwachanganya wateja jambo ambalo halikubaliki kisheria.
Moses Mbunda ni Mwanasheria wa Wakala wa Vipimo. Yeye anafafanua kuwa kuhusu madhumuni ya kanuni hiyo kuwa ni kuhakikisha kuwa biashara ya gesi hapa nchini inafanyika kwa haki na hivyo kuwalinda watumiaji.
“Kanuni hiyo mpya inataka makampuni na wafanyabiashara wa bidhaa hiyo kuzingatia kuwa, vipimo vyote vitakavyotumika ni vile vinavyotumia mfumo wa kimataifa (SI units) ambavyo nchi yetu imeridhia,” anasema. Anaongeza kuwa mfumo huu wa vipimo utumike hususani katika kuelezea uzito wa mtungi ulio tupu (tare weight), uzito wa gesi peke yake (net weight) na ule uzito wa mtungi na gesi (gross weight).
Mbunda anasema kanuni hiyo inabainisha kuwa mtungi uliobeba gesi ni sharti uwe na maandishi yanayoonesha utambulisho wa bidhaa hiyo, jina la kampuni inayosambaza, namba ya mtungi, uzito wa mtungi bila gesi, uzito wa gesi peke yake na uzito wa mtungi pamoja na gesi.
Kanuni hiyo pia inawataka wafanyabiashara wa gesi iliyofungashwa kwenye mitungi kuwa na mizani katika kila eneo la biashara kwa ajili ya kuhakikisha uzito wa bidhaa hiyo pindi mteja anapokuwa amenunua.
Wakaguzi kutoka Wakala wa Vipimo watapita kila eneo la biashara kukagua kama mfanyabiashara huyo anayo mizani iliyothibitishwa na Wakala wa Vipimo na kwamba kanuni zote zinazotakiwa kuwa zimezingatiwa katika ufungashaji wa bidhaa hiyo. Mbunda anasema Wakala wa Vipimo utasimamia ipasavyo, utekelezaji wa kanuni hiyo mpya kwa lengo la kuwalinda watumiaji.
 
© 2012. Design by Ernest James Siwigo Chambasi - Supported By John James Chambasi And Maganza Family