WAHAMIAJI HARAMU KURUDI TANZANIA


BAADA ya kukaa bila waume na wake kwa zaidi ya mwezi mmoja sasa kutokana Operesheni Kimbunga, Serikali imetangaza kuwa itatoa fomu maalumu ili kuwarejesha nchini wahamiaji haramu walioolewa au kuoa nchini ili waungane na familia zao.
Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta aliyasema hayo mjini hapa alipokuwa akizungumza na waumini wa Kanisa Katoliki waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa kanda ya Mungu ni Mwema ya Kwaya ya Kapotive ya mjini Bukoba. Waziri Sitta alisema;
“Serikali imeamua sasa kwamba watarudi nchini lakini watajaza fomu maalumu za kuwawezesha kuishi ili waungane na familia zao na kuendelea kufurahia maisha ya ndoa na familia.
“Tumeona tufanye hivyo kwani si kazi ya serikali kuvunja ndoa za watu. Lakini katika kuchukua hatua hiyo tutakuwa makini kuhakikisha kuwa wahamiaji wahalifu hawarejei nchini,” alisema. Alisema,
“Nawahakikishia kuwa enzi wa wahalifu sasa basi. Rais (Jakaya Kikwete) hakutangaza operesheni hii hivi hivi, bali alichoshwa na matukio ya uhalifu yaliyokuwa yanatokea.
“Enzi za wananchi wetu kushushwa kwenye mabasi na kuporwa, misitu yetu kuvamiwa na wahamiaji hawa wakiwa na idadi kubwa ya mifugo na pia vijiji vyetu kuvamiwa na wageni na kutumia fedha zao, kufundisha kwa mitaala yao na kupeperusha bendera za nchi zao ndani ya Tanzania sasa basi,” alisema Sitta.
Kauli ya Sitta inakuja baada ya kuwepo kwa malalamiko hasa katika maeneo ya mipakani kwa operesheni kimbunga, kusababisha ndoa nyingi kuvunjika, kutokana na wanaume au wanawake waliooa au kuolewa nchini kukumbwa na operesheni kimbunga na kuziacha familia zikiteseka.
Mkuu wa Wilaya ya Ngara, Constatine Kanyasu alimwambia Sitta alipotembelea mpaka wa Rusumo hivi karibuni, kwamba wanaume wengi wa Tanzania wanaoa Rwanda kutokana na mahari kuwa ndogo kuliko wakioa Watanzania na pia kutokana na Wanyarwanda kuwa na sura na maumbo ya kuvutia.
Hata hivyo, Mkuu huyo wa Wilaya alisema pamoja na kufurahishwa na hayo lakini wanandoa hao wamekuwa wakishindwa kulipa ada ya Dola za Marekani 550, zinazotozwa kila baada ya miaka miwili ili kuwawezesha wenzi wao kuishi kwa mujibu wa sheria.
Akizungumzia uzinduzi wa kanda hiyo, Sitta aliwaasa wanakwaya nchini kutumia nyimbo kuonya juu ya kuporomoka kwa maadili nchini akisema vijana wanateketea kwa kubebeshwa dawa za kulevya na watu wenye fedha na madaraka.
“Maadili yameshuka sana ndani ya nchi yetu, vijana wetu sasa wamegeuzwa kuwa punda wa kubeba dawa za kulevya. Hadi sasa vijana zaidi ya 600 wamefungwa Brazil, Singapore, Malaysia, China, Marekani na Afrika Kusini huku baadhi wakisubiri kunyongwa, wanakwaya tumieni nafasi hii kuomba Mungu atuepushe na janga hili,” alisema Waziri Sitta.
Alisema janga hilo linachangiwa kwa kiasi kikubwa na kutafuta utajiri wa haraka huku akiongeza kwa kusema; “Sisi wazee ndio tunaopaswa kulaumiwa kwa kuwaingiza vijana katika kutafuta utajiri wa dhambi kwa kutokuwa na roho ya huruma na kuifanya nchi kupoteza taswira nzuri katika anga za kimataifa,” alisema.
 
© 2012. Design by Ernest James Siwigo Chambasi - Supported By John James Chambasi And Maganza Family