PAULSEN AAHIDI UBINGWA CHALLENGE

Kim-Poulsen_18f0d.jpg
Kikosi cha timu ya Taifa ya Tanzania Bara 'Kilimanjaro Stars' kimeondoka jana jioni kwenda nchini Kenya kwa ajili ya mashindano ya Chalenji kikiwa na lengo moja la kutwaa ubingwa.
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam wakati timu hiyo ikikabidhiwa Bendera ya Taifa na Katibu Mkuu wa Baraza la Michezo Tanzania, Henry Lihaya, Kocha mkuu wa Kilimanjaro Stars, Kim Poulsen alisema wanaondoka nchini wakiwa na nia ya kutwaa ubingwa wa mashindano hayo, lakini lengo lake la kwanza ni kuhakikisha timu hiyo inafuzu kutoka hatua ya makundi na kuingia hatua ya mtoano.
Alisema baada ya kuvuka hatua hiyo lengo lake la pili ni kupambana vilivyo ili kuhakikisha wanaibuka mabingwa wa mashindano hayo kama ilivyokuwa mwaka 1994, ambapo timu hiyo ilinyakua kombe hilo nchini Kenya.(P.T)
Katika mashindano hayo, Kilimanjaro Stars ipo kundi B na timu za Zambia, Burundi na Somalia, ambapo itacheza mechi yake ya kwanza dhidi ya Zambia, Novemba 28 mwaka huu kwenye Uwanja wa Machakos.
Poulsen alisema anaamini kuwa watakumbana na ushindani mkubwa, lakini hiyo ndiyo itakuwa nafasi kwa wachezaji wake kupigana vilivyo na wale chipukizi ndiyo wakati wao wa kumwonyesha kuwa wanaweza. Pia hii ndiyo tiketi ya kujitangaza kimataifa wakati wale wakongwe ndiyo muda wao wa kumwonyesha kuwa wanastahili kuendelea kubakia katika kikosi hicho na kile cha Taifa Stars.
"Pia mashindano hayo nitayatumia kwa ajili ya kuangalia wachezaji watakaounda kikosi cha Taifa Stars kutoka Tanzania Bara na Zanzibar ambao wataiwakilisha Tanzania katika harakati za kutafuta tiketi ya kufuzu kushiriki fainali za Afrika 2015," alisema Poulsen.
Naye Lihaya aliwataka wachezaji wa Kilimanjaro Stars kwenda kupambana na kuhakikisha wanafanya vizuri na kurejea nchini wakiwa na kombe.
 
© 2012. Design by Ernest James Siwigo Chambasi - Supported By John James Chambasi And Maganza Family