BUNGE KUANZA DODOMA LEO

MKUTANO wa 13 wa Bunge unaanza leo mjini hapa, ambapo pamoja na mambo mengine, unatarajia kujadili Miswada ya sheria mbalimbali, ukiwamo ule wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa Mwaka 2013.
Aidha, miswada mingine inayotarajiwa kujadiliwa na wabunge katika mkutano huo ni Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali na ule wa Kura ya Maoni wa Mwaka 2013.
Katika mkutano wake na waandishi wa habari jana Kaimu Mkurugenzi wa Habari, Elimu kwa Umma na Uhusiano wa Kimataifa wa Bunge, Deogratias Egidio, alisema Serikali imesema itaupeleka bungeni Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa Mwaka 2013 kwa ajili ya kujadiliwa katika Mkutano wa Bunge wa sasa.
Hata hivyo, Egidio alisema hadi jana Bunge lilikuwa bado halijapokea muswada huo. Alisema kutokana na mabadiliko ya kalenda ya Mkutano wa Bajeti ya Serikali na pia kwa mujibu wa Kanuni ya 94 ya Kanuni za Bunge toleo la 2013, Bunge litakaa kama Kamati ya Mipango ili kutekeleza matakwa ya Ibara ya 63(3) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Alisema Ibara hiyo, inalipa uwezo Bunge kujadili na kuishauri Serikali juu ya mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2014/2015. Bunge linategemewa kuujadili Mpango huu kwa siku tano mfululizo.
Alisema Bunge linaweza pia kufanya shughuli nyingine yoyote, kama litajiridhisha kuwa inakidhi kanuni zake.
Aidha miongoni mwa mambo yaliyotarajiwa kuwamo kwenye orodha ya shughuli za Mkutano wa sasa wa Bunge na kujadiliwa na wabunge ni Muswada binafsi, uliowasilishwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (Chadema) ambaye anataka Sheria ya Magazeti ya Mwaka 1976 ifutwe.
Egidio alisema katika Mkutano wa sasa wa Bunge, kutakuwa na maswali ya kawaida ya msingi 125 na 16 ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu, yatakayoulizwa na wabunge. ***************************************
 
© 2012. Design by Ernest James Siwigo Chambasi - Supported By John James Chambasi And Maganza Family