HABARI KAMILI KUHUSU MBWA ALIYEKUTWA NA MGUU WA MTU MKOANI MBEYA

IMANI za kishirikina zimezidi kukitisa Kijiji cha Isange, Kata ya Isange, Wilaya ya Rungwe, mkoani Mbeya baada ya matukio ya kupotea na kuuawa kwa watoto kutokea mara kwa mara ambapo safari hii binti mmoja wa darasa la saba ameuawa na mguu wake kukutwa ukiliwa na mbwa.
Binti huyo aliyeuawa amegundulika kuwa ni mwanafunzi wa darasa la saba  aliyejulikana kwa jina la Lista Sebule aliyekuwa akisoma katika Shule ya Msingi Mpombo iliyopo Isange na alipotea katika mazingira ya kutatanisha na maiti yake kukutwa kando ya mto siku tisa baadaye. Katika tukio la awali, mtoto mmoja alikatwa kichwa na watu wasiojulikana kisha kutoweka nacho.
Mama mzazi wa marehemu, Christina Sakalile alisema binti yake (Lista) alipotea saa tisa jioni ya Machi 31, mwaka huu baada ya kutumwa kupeleka simu kibandani ili ‘ikachajiwe’ lakini hakurudi hadi giza lilipoingia, hali iliyozua wasiwasi na wakaanza kumtafuta bila mafanikio.
“Baada ya tukio hilo, Mwenyekiti wa Kitongoji cha Isange, Daudi Nsyani aliitisha mkutano wa wananchi wote ili mtoto atafutwe. Juhudi hizo zilizaa matunda Aprili nane, mwaka huu lakini alipatikana akiwa amekufa huku akiwa hana baadhi ya viungo mwilini,” alisema mama huyo huku akitokwa machozi.
  Mashuhuda wa tukio hilo walisema mwili wa marehemu ulipatikana ukiwa kando ya Mto Nkalisi uliopo kijijini hapo ukiwa umekatwa kichwa na miguu ambapo mguu mmoja ulipatikana baada ya mbwa kukutwa akiwa anaula na alipoona watu akawa anakimbia nao.
Hali hiyo iliwafanya watu kumfuatilia mbwa huyo ambaye aliongoza hadi kwenye mwili wa marehemu na kuwakuta mbwa wengine wawili wakiwa kando yake ambapo uongozi wa kijiji uliliarifu jeshi la polisi.
“Polisi walipofika walifanya uchunguzi na wananchi wakapiga kura ya siri ambapo watu wawili walikamatwa wakituhumiwa kuhusika na tukio hili. Mwili ulikabidhiwa kwa ndugu na wakauzika siku hiyohiyo na mazishi yake yaliweka historia kwa kuhudhuriwa na watu wengi,” alisema shuhuda huyo.
Diwani wa Kata ya Isange, Elias Mwandele amethibitisha kutokea tukio hilo na aliwataka wazazi kutowapeleka watoto kwenye shughuli za kuchunga mifugo kwa sasa.
(Habari, picha na Mbeya Yetu)

 
© 2012. Design by Ernest James Siwigo Chambasi - Supported By John James Chambasi And Maganza Family