![]() |
| Mabaki ya Mizoga ya Tembo waliouawa hifadhini. Picha Katunews. |
Na Zitto Kabwe
MWAKA mzima uliopita, 2012, ulijaa habari za
kukamatwa kwa shehena za meno ya Tembo kutoka Tanzania huko HongKong
zikielekea China. Mwezi Disemba shehena yenye tani 1.3 ya meno ya Tembo
iliyofichwa kwenye magunia ya Alizeti ilikamatwa na Maafisa wa Forodha
wa Hong Kong. Shehena hii ilikuwa na thamani ya dola za kimarekani
milioni moja na nusu. Wiki mbili kabla ya hapo takribani tani nne za
meno ya Tembo zilikamatwa huko huko HongKong. Kwa matukio haya mawili,
hawa ni sawa na Tembo 900 waliouwawa.
Mwezi huo huo wa Desemba, 2012 Polisi mkoani Arusha walikamata nyara
nyingi za Serikali katika eneo la Kisongo. Nyara hizi ni pamoja na
ngozi za Simba na wanyama wengine, pembe za ndovu na wanyama wengine na
vichwa vya wanyama. Nyara hizi zilikuwa tayari kwa kuuzwa nje ya Nchi.
Mkoani Katavi walikamatwa majangili kadhaa na kuachiwa huru kwa amri
kutoka juu kwa mujibu wa taarifa za maafisa wa wanyama pori.
Ujangili umeshamiri sana na kwa kasi ya kutisha. Takwimu za Serikali
zinaonyesha kuwa mwaka 2010 jumla ya Tembo 10,000 waliuwawa hapa
Tanzania peke yake. Hii ni sawa na Tembo 37 kila siku. Hali imekuwa
mbaya zaidi mwaka 2012 ambapo jumla ya Tembo 23,000 waliuwawa sawa na
wastani wa Tembo 63 kila siku. Kwa hesabu ya haraka, kutokana na kasi
hii ya ujangili, ifikapo mwaka 2017/2018 Tanzania haitakuwa na Tembo
hata mmoja. Hivi sasa Tanzania ina Tembo kati ya 150,000 na 170,000.
Maafisa wengine wa Wanyama pori wanasema Tembo wanafika 250,000 na nusu
ya Tembo hao wapo pori la Selous kusini mwa Tanzania. Sote tuna wajibu
wa kulinda urithi huu tulioachiwa na MwenyeziMungu.
Kasi ya ujangili imechangiwa na mambo mengi sana lakini kubwa ni
kukua kwa uchumi wa China na nchi nyingine za Kusini Mashariki mwa
Asia. Kwa hiyo takribani nchi zote za Afrika zenye Tembo zinaathirika
na Biashara hii ya Pembe za Ndovu. Tanzania, Kongo-Kinshasa na Msumbiji
zipo kwenye hatari zaidi ya Tembo wake wote kumalizika kutokana na
nguvu kubwa waliyonayo wafanyabiashara haramu wa Pembe za Ndovu. Kenya
na Nigeria inasemekana jumla ya Tembo 25,000 waliuwawa mwaka 2011 peke
yake. Inasemekana kuwa kuongezeka kwa wafanyabiashara wengi kutoka
China na hivyo wafanyakazi kwenye makampuni ya Kichina kuzagaa Afrika
kunachangia kwa kiasi kikubwa sana Ujangili na biashara hii haramu.
![]() |
Pembe
za ndovu zilizokamatwa katika operesheni dhidi ya biashara ya magendo
huko Hong Kong zikioneshwa kwenye mkutano wa vyombo vya habari.
|
Mtandao wa Ujangili ni mpana na wenye nguvu sana za pesa, kisiasa na kimamlaka. Mtandao huu huanzia chini kabisa kwenye Mapori na Hifadhi ambapo wauaji ni watu masikini wa vijijini na wengine hutumia magobole tu. Hawa hulipwa kwa kuua tu. Wakataji nao huingia hapo na kukata meno na kuandaa usafiri ambao hufanywa wakati mwingine na magari ya Serikali. Hivi karibuni gari za polisi, muhimbili na hata magari ya viongozi wa dini yamekamatwa na meno ya Tembo huko mkoani Iringa. Baada ya kusafirishwa na kufikishwa maeneo ya mijini hufungwa na kusafirishwa kupitia bandari ya Dar es Salaam. Katika mtandao huu kuna watu wa Vijijini, masikini ambao hutumia ujangili kama sehemu ya kupata kipato. Pia kuna watu wa kati kama maafisa wa Polisi, maafisa wa wanyama pori, madereva wa magari ya Serikali wenye tamaa tu kuongeza kipato. Juu kabisa kuna wafanyabiashara wakubwa na inasemekana pia wanasiasa ambao hulinda biashara hii.
Nina karibia kumaliza kitabu cha kurasa 301 kiitwacho “Killing for
Profit: Exposing the illegal Rhino Horn Trade” ambacho kimeandikwa na
Mwandishi wa habari Julian Rademeyer wa Afrika Kusini. Kitabu hiki ni
cha uchunguzi ambapo mwandishi amechunguza mtandao mzima wa biashara
haramu ya meno ya Faru. Mwandishi anasema, kule nchi za Kusini
Mashariki mwa Asia kama Vietnam, meno ya Tembo na Meno ya Faru yana bei
kubwa kuliko dhahabu na madawa ya kulevya. Anasema Biashara hii imejaa
tamaa za mali na rushwa ya kiwango cha juu. Mwandishi anaonyesha kwa
ushahidi namna biashara hii ilivyotumika kuendeleza vita Msumbiji na
Angola kwa nguvu ya Serikali ya Makaburu. Hata baada ya ukaburu kuisha
anaonyesha namna ambavyo wanasiasa watawala wanaendeleza biashara hii
na kupata fedha za kampeni.
Katika kitabu hiki Mwandishi anathibitisha kuwa Meno ya Tembo na
Meno ya Faru huko Asia hutumika kama mapambo kwa kutengeneza bangili
zenye bei aghali na kwa matajiri na mapambo mengine kwenye mikufu,
herein nk. Hata hivyo anasema meno haya hutumika kama dawa na hasa dawa
za kuongeza nguvu za kiume kwa wanaume na hivyo kusababisha bei yake
kuwa kubwa sana. Jinsi uchumi wa Mataifa hayo unavyokuwa na kuongeza
watu wa tabaka la kati, ndivyo mahitaji wa Meno ya Tembo na Faru
yanaongezeka. Mwandishi anaonyesha kwamba mwaka 1960 kulikuwa na Faru
100,000 katika nchi za Zimbabwe na Afrika Kusini. Hivi sasa kuna Faru
2400 tu. Nadhani ni muhimu kupata pia takwimu za Tanzania kuonyesha
hali upande wetu ipoje. Watafiti waliofanya tafiti kwenye eneo hili
watujuze.
Jambo moja lipo wazi hapa Tanzania ni kwamba maeneo ya Hifadhi za
Taifa takwimu za Ujangili ni chache kuliko maeneo ya mapori ya Akiba
kama Selous. Hii inatokana na ukweli kwamba maeneo ya mapori ya Akiba
uwezo wan chi kulinda wanyama ni mdogo sana maana hakuna askari wa
kutosha na waliopo maslahi yao ni madogo sana. Hivyo moja ya pendekezo
la dhati kabisa ni kuimarisha ulinzi kwenye mapori ya Akiba. Pori kama
Selous ambalo ni urithi wa Dunia ni vema liundiwe mamlaka yake (Selous
Games Authority) kama ilivyo Mamlaka ya Ngorongoro. Mapori mengine
yawekwe chini ya wakala wa Serikali na yawezeshwe kutokana na mapato ya
uwindaji wa Kitalii. Lazima kutoa motisha ya kutosha kwa Askari wa
wanyama pori na pia kutoa adhabu kali sana kwa askari atakayejihusisha
na ujangili.
Hata hivyo, wataalamu wa wanyamapori wanasema ‘kuua majangili
hakuleti mafanikio yeyote. Kuna watu wengi sana masikini wapo tayari
kuingia kuua Tembo ili wapate pesa kidogo. Hata ukiua mamia yao,
hawatamalizika. Suluhisho pekee ni kuua soko la biashara hii haramu’.
Soko hili litakufa kwa kuusambaratisha mtandao wa ujangili kwa kuanzia
na wafanyabiashara wakubwa. Hii ndio opresheni. Operesheni linda Tembo.
Sasa ianze. Tafuta namba ya simu ya Mbunge wako au mbunge yeyote
mwandikie “nataka ulinde Tembo wetu kwa kuihoji na kuiwajibisha
Serikali”. Mabadiliko ni Mimi, Ni wewe, Ni sisi. Tumia simu yako kutaka
viongozi wako wawajibike. Ni wajibu wetu kikatiba kulinda urithi wetu.
Short URL: http://www.thehabari.com/?p=27534


