TIMU ZA UKANDA WA CECAFA ZANG`ARA

Yanga imeweka rekodi ya kufunga mabao saba na kuziongoza klabu za Ukanda wa Afrika Mashariki kuanza kwa kishindo michuano ya Ligi ya Mabingwa  na Kombe la Shirikisho Afrika.
Mabingwa wa Tanzania Yanga, waliitungua Komorozine ya Comoro mabao 7-0 ambao ni ushindi mkubwa zaidi kwa matokeo ya mechi zote za ufunguzi zikiwamo za Ligi ya Mabingwa na Kombe la Shirikisho zilizopigwa Februari 7, 8 na 9.
Katika michuano ya Ligi ya Mabingwa, Afrika Mashariki  inawakilishwa na timu sita.
Miongoni mwa timu hizo sita ni KMKM ya Zanzibar pekee ndiyo ilipoteza mchezo wake katika mechi hizo baada ya kukung’utwa mabao 3-0 na Dedebit ya Ethiopia, wakati nne zilishinda na moja ilitoka suluhu.
Timu zilizovuna ushindi ni Gor Mahia ya Kenya iliyoidungua 1-0 US Bitam ya Gabon, Yanga ikaizaba Komorozine mabao 7-0, Flambeau de l’EST ilipata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Diables Noirs ya Congo, KCCA iliikandamiza El Merrikh ya Sudan mabao 2-0, wakati Rayon Sports ililazimishwa suluhu na AC Leopards ya Congo.
Kwa upande wa Kombe la Shirikisho, Ukanda wa Afrika Mashariki,  pia unawakilishwa na timu sita, ambapo Chuoni ya Zanzibar walifungwa mabao 2-0 na How Mine ya Zimbabwe, Academie Tchite ya Burundi ililazwa bao 1-0 na AS Kigali ya Rwanda na Victoria University ya Uganda iliyobonyezwa mabao 3-0 na Don Bosco ya DR Congo.
AFC Leopards ya Kenya iliichapa  2-0 Defence ya Ethiopia, Azam ya Tanzania iliizaba Ferroviario ya Msumbiji bao 1-0.
 
© 2012. Design by Ernest James Siwigo Chambasi - Supported By John James Chambasi And Maganza Family