![]() |
RAIS Jakaya Kikwete amesema serikali imetenga Sh bilioni 21 katika
bajeti ya mwaka wa fedha wa 2014/2015 kwa ajili ya kumaliza tatizo la
upungufu wa vitabu kwenye shule za sekondari.
Kauli hiyo ameitoa wakati akihutubia wananchi wa kata ya Kimbe baada
ya kuweka jiwe la msingi kwenye maabara ya masomo ya sayansi ya
sekondari ya kata hiyo ambapo ujenzi wake utagharimu jumla ya Sh milioni
135 hadi kukamilika.
Mpaka sasa ujenzi wa maabara hiyo ya masomo ya fizikia, kemia na
baolojia ulioanza mwaka jana umegharimu Sh milioni 59 . Kati ya hizo
mchango wa wananchi ni Sh milioni 47.4, halmashauri Sh milioni 12.5 na
kiasi kilichobaki ni mchango wa serikali kuu.
Ujenzi utakamilika Novemba mwaka huu. Rais alisema fedha hizo
zimeongezwa ili kukabiliana na uhaba wa vitabu vikiwemo vya masomo ya
baolojia, kemia, fizikia na hisabati ili kuwawezesha wanafunzi wanaosoma
katika shule za sekondari hususan za Kata kujifunza masomo ya sayansi.
“Katika mwaka ujao wa fedha tumeamua kuongeza fedha tunazotenga kwa
ajili ya ununuzi wa vitabu na lengo hasa la serikali ni kupunguza tatizo
lililopo sasa pamoja na kuboresha mazingira ya kujifunzia”, alisema.
Aliongeza, “lengo la kuhakikisha msisitizo katika kuboresha mazingira
ya utoaji elimu, hasa kwa kuongeza idadi ya wanafunzi wanaosoma masomo
ya Sayansi ni kuwezesha kata kupata wataalamu wenye ujuzi katika fani za
sayansi ikiwemo Afya, Uhandisi, Madaktari ambao watasaidia kuchochea
maendeleo ya jamii husika na taifa kwa ujumla”, alisema.
Aidha, alisema serikali inatambua tatizo la uhaba wa nyumba za walimu
na kwamba tayari imetenga Sh milioni 500 kwa kila halmashauri nchini
kupunguza tatizo hilo.
“Kwa kutambua umuhimu wa shule za sekondari za kata serikali imeamua
kutenga Sh milioni 500 kwa kila halmashauri kuendeleza mpango wa ujenzi
wa nyumba za walimu ambao utaboresha mazingira yao ya kazi na kuongeza
uhakika wa walimu shuleni”.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi, Daudi Mayeji
akizungumzia utekelezaji wa Mpango wa dharura wa serikali wa
kukabiliana na uhaba wa maabara alisema kwa Kilindi tayari halmashauri
imenunua maabara nne zinazotembea zenye thamani ya Sh milioni 10 mwaka
huu wa fedha.
Awali Mbunge wa Kilindi, Beatrice Shelukindo alimweleza rais kuwa
tatizo kubwa linalowakabili wananchi wake ni bei ndogo ya mazao hasa
mahindi ambapo wakati wa msimu wa mavuno debe moja linauzwa kwa Sh
2,400.
Akijibu ombi hilo rais alisema atawaelekeza wakala wa taifa wa
ununuzi wa mazao wenye ofisi zao wilayani Handeni (NFRA) kununua mahindi
ya wakulima wa wilayani Kilindi ili kuwawezesha kujikwamua ki uchumi.
|
